Habari
SERIKALI YATOA WITO KWA WADAU KUWEKEZA KATIKA SEKTA ZA KILIMO NA VIWANDA

Serikali ya Tanzania imehimiza wadau wa maendeleo kuunga mkono jitihada zake za kukuza sekta za kilimo na viwanda vya uzalishaji.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji, Prof. Kitila Alexander Mkumbo(Mb.), alitoa wito huu katika mazungumzo kati ya serikali na wadau hao jijini Dodoma.
Prof. Mkumbo alisisitiza kuwa nchi zilizoendelea zilipitia mapinduzi katika kilimo na viwanda vya uzalishaji. "Tunawaalika tushirikiana na serikali kuwekeza katika kilimo na viwanda vya kuongeza thamani," amesema.
Prof. Mkumbo alibainisha kuwa serikali imefanya maboresho ya kisera na kisheria ili kuboresha mazingira ya biashara na uwekezaji. Ameongeza kuwa Tanzania ina idadi kubwa ya vijana, hivyo kukuza sekta za uzalishaji na ajira ni kipaumbele muhimu.
"Elimu na viwanda vya uzalishaji vitakuwa msingi wa mipango na utekelezaji wa shughuli za kiuchumi katika Dira ya Maendeleo ya Taifa ya 2050, ili kuzalisha ajira kwa vijana hawa," alisema.